WB, GCA WASHIRIKIANA KUTOA MAFUNZO ELEKEZI YA KUKABILIANA NA MABADILIKO YA HALI YA HEWA

Benki ya Dunia (WB) kwa kushirikiana na Global Climate Adaption (GCA) imetoa mafunzo elekezi ya kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa (Climate Adaption) kwa wadau wa Sekta ya Kilimo wanaotekeleza Programu ya Mifumo Himilivu ya Chakula Tanzania (TFSRP) tarehe 17 na 18 Machi 2025, Ukumbi wa Nashera jijini Dodoma.
Lengo la mafunzo ni kujenga uelewa wa pamoja kuhusu utoaji wa huduma za ugani na mifumo ya upatikanaji wa pembejeo ikiwemo mbegu kwa Wataalamu kutoka Wizara ya Kilimo na Taasisi zake, Taasisi ya Kilimo ya Kimataifa ya Mabadiliko ya Tabia Nchi (IITA), Kampuni inayohusika kutoa Taarifa za Masoko kwa Wakulima Kidigitali (ESOKO), Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) pamoja na Kituo cha Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi Duniani yaani "Global Climate Adaption” (GCA).
Mafunzo haya yalijikita katika kutoa dira ya kumfikia mkulima mdogo katika ukusanyaji na utoaji wa taarifa za hali ya hewa na masoko kupitia teknolojia (ikiwemo kupitia simu za mkononi) pamoja na kuwahusisha wadau wa kibiashara wa masuala ya ugani kwa njia ya kidigitali.
Wizara ya Kilimo inaendelea na utekelezaji wa Programu ya Mifumo Himilivu ya Chakula katika maeneo ya utoaji huduma za kilimo ili kuhamasisha matumizi ya teknolojia na mbinu zinazohimili mabadiliko ya tabianchi kupitia tafiti za mbegu bora. Tafiti zinafanywa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI) ambapo pia programu ya TFSRP inatoa huduma za ugani ikiwemo zoezi la upimaji wa afya ya udongo kupitia uwekezaji wa fedha katika Sekta ya Kilimo.